Na. Sizah Kangalawe, DODOMA
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule amewahimiza madereva wa Serikali kutumia vyema mafunzo waliyopatiwa katika kuboresha utendaji kazi wao na kuleta tija zaidi.
Alitoa maagizo hayo Septemba 04, 2025 jijini Dodoma wakati akifunga Kongamano la Nne la Chama cha Madereva wa Serikali Tanzania (CMST) lililofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete.
"Naamini mada mlizofundishwa hapa zitakwenda kuboresha uwezo wenu katika utendaji kazi na kuleta tija zaidi katika kuhakikisha mwajiri mkuu ananufaika na mafunzo mliyopata kupitia kongamano hili, na ninaamini kuwa kushiriki kwenu kutapelekea kuendesha magari kwa ustadi na kupunguza matukio ya ajali. Tutajua thamani ya abiria mliowabeba na kuendesha tukiwa tunawakinga na madhara, lakini pia mtajua thamani ya vitu mnavyobeba kupitia magari hayo ambayo mnatakiwa mvisafirishe kwa usalama,” alisema Senyamule.
Alifafanua kuwa madereva wa Serikali ni mhimili muhimu katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku ya Serikali kwani ndio wanaohakikisha usafiri wa viongozi na watumishi unakuwa salama, wenye ufanisi na unaoendana na hadhi ya Taifa la Tanzania.
Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi, Dkt. Charles Msonde, alisema Serikali imeboresha muundo mpya wa madereva ambao pia unasimamia maboresho ya mishahara na stahiki nyingine kwa madereva wa Tanzania Bara.
Kongamano hilo lililoandaliwa na CMST, limefanyika kwa siku tano ambapo lilianza Agosti 31 na limetamatika Septemba 04, 2025 huku likienda sambamba na kaulimbiu "Dereva wa Serikali, epuka ajali, linda gari lako na watumiaji wengine wa barabara, shiriki uchaguzi mkuu Oktoba 2025."
Chama cha Madereva wa Serikali kilianzishwa mwaka 2013 na kusajiliwa Wizara ya Mambo ya Ndani mwaka 2015 kwa Na. ya Usajili S.A. 20314, ambapo hadi sasa kina jumla ya wanachama zaidi ya 3,500.
1 CDA Street, 40477
Anuani ya posta: 1249, DODOMA, TANZANIA
Simu: +255 26 232 4817
Simu ya kiganjani:
Baruapepe: cd@dodomacc.go.tz
Copyright ©2017 The City Council of Dodoma. All rights reserved.