Na. Shahanazi Subeti, DODOMA
Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) pamoja na Halmashauri ya Jiji la Dodoma zilisaini mkataba wa TACTIC wenye thamani ya shilingi Bilioni 14.2 kwa lengo la kuboresha miundombinu, kuimarisha usimamizi wa uendelezaji miji na kuboresha mazingira ya uwekezaji ili kukuza uchumi wa halmashauri ya jiji.
Hafla hiyo ya Utiaji saini ilifanyika bustani ya Chinangali Park jijini Dodoma katika hafla ya utiaji saini mkataba wa ujenzi wa soko kuu la majengo pamoja na ujenzi wa kituo cha daladala eneo la Mshikamano, Kizota na Nzuguni.
Akielezea tukio hilo Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mohamed Mchengerwa alisema, mikataba hii itakwenda kuleta mapinduzi makubwa ya kiuchumi kwa watanzania wanaoishi Dodoma na aliwaomba wakandarasi kutekeleza majukumu yao kwa wakati. "Tunapoboresha miundombinu hii itawafanya watanzania na wafanyabiashara, kuweza kusogeza biashara zao karibu, kuweza kutumia vivuko, madaraja na barabara ambazo tumekwisha saini hapa, matarajio yetu usimamizi wa miradi hii kwa kila mmoja wetu anajukumu la kuitunza kwa sababu gharama inayotumika ni kubwa sana. Nina muelekeza Mkandarasi ambae tumesaini leo mkataba nenda kafanye kazi usiku na mchana ili kukamilisha muda uliopangwa na hakutakuwa na nyongeza ya muda" alisema Mchengerwa
Sambamba na hilo, alimpongeza Rais kwa kuweza kulijenga jiji "ameyafanya mengi ndani ya muda mfupi na sisi wasaidizi wake wa karibu kuna wakati tunajiuliza fedha hizi zinatoka wapi, miaka 10 iliyopita hatukuwa na barabara za lami wala majengo makubwa makubwa, tulianza na ujenzi wa Ofisi za serikali lakini Rais akaamua kujenga maghorofa katika mji wa serikali na sasa akaona upo umuhimu wa kwenda kuboresha majiji na miji, akatafuta fedha akatuelekeza wasaidizi wake kuhakikisha tunakwenda kuzisimamia ili Dodoma iwe makao makuu ya nchi yetu" alisema Mchengerwa
Pia aliwataka wananchi wa Dodoma kumpongeza sana Mbunge wao kwa kazi kubwa anayoifanya kwa kutatua kero katika mitaa yao "kila mmoja unaemsikia hapa amezungumza Kwa kina na aliwazungumzia wananchi wake amegusa kila kata na amesema kuhusu changamoto kadhaa ambazo madiwani wa nchi wanakutana nazo hasa madiwani wa Dodoma na nimepokea changamoto hizi na kwakuwa kwenye wizara hii Rais mwenyewe nitaziwasilisha kwake" alisema Mchengerwa.
Kwa upande wake wakala wa Barabara za mijini na vijijini ( TARURA) mhandisi Victor Seif alisema Halmashauri ya Jiji la Dodoma, awamu ya kwanza kazi zinazofanyika ni ujenzi wa Barabara za mijini katika ( Km 13.0) na ujenzi wa jengo la usimamizi na uratibu wa miradi pia katika awamu ya pili kazi zinazofanyika katika mkataba ni pamoja na uboreshaji wa Soko Kuu la Majengo, kituo Cha daladala eneo la Mshikamano, uboreshaji wa stendi ya mabasi madogo eneo la Kizota, ujenzi wa stendi ya mabasi madogo eneo la Nzuguni, ujenzi wa vivuko maji(footbridges) katika maeneo ya Chaduru, Maili mbili na Ntyuka.
Alisema kuwa miradi hiyo kwa awamu zote mbili unasimamiwa na mshauri elekezi ambae ni M/S Hong- IK Engineering consultants CO.ltd in association with gauge pro consult(T) ltd.and G and Y engineering consult PLC, kwa gharama ya mkataba wa usimamizi ni Milioni 667,100,000.00 "katika hatua ya utekelezaji awamu ya kwanza mradi umefikia asilimia 37.7 ya utekelezaji ( malengo ya utekelezaji ni kufikia asilimia 88.6 Mpaka mwisho wa mwezi Desemba, 2024 hivyo mkandarasi wa ‘package 1’ yupo nyuma kwa asilimia 59.9. Kwa awamu ya pili ni kuanza utekelezaji tarehe 1/2/2025 kwa mkataba wa miezi 12. Pia utekelezaji unafuata mpango wa manunuzi ulioidhinishwa katika andiko la mradi ‘project appraisal document’ pamoja na makubaliano ya utekelezaji ‘financing agreement’ kati ya serikali kuu na Benki ya Dunia" alisema Seif.
Kwa upande wake, Mbunge wa Dodoma, Anthony Mavunde, alisema kuwa miradi hii imeleta mageuzi na mapinduzi sana kwa kuleta maendeleo katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma" naishukuru sana serikali kwa mradi ambao leo tunakwenda kutia saini mradi ambao una thamani zaidi ya shilingi Bilioni 24.0 ukiwa ni awamu ya kwanza ya mradi wa kundi la kwanza ‘tier 1’ ambapo tunaamini kabisa kupitia miradi huu tutakwenda kuleta mapinduzi makubwa ya kusaidia kutatua changamoto za miundombinu ndani ya Jiji letu la Dodoma na hii ni awamu ya pili ambayo tunasaini leo una thamani ya Bilioni 14.2 mradi huu unaenda kufanya yafuatayo kuboresha Soko Kuu la Majengo pamoja na kituo cha daladala eneo la Mshikamano, uboreshaji wa stendi ya mabasi madogo eneo la Kizota, ujenzi wa stendi ya mabasi madogo eneo la Nzuguni na ujenzi wa vivuko maji (footbridges) katika maeneo ya Chaduru, Mailimbili na Ntyuka" alisema Mavunde.
Pia aliongezea Kwa kumshukuru Raisi wa jamhuri ya muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan Kwa kuwezesha Dodoma kuwa na miradi mikubwa ya kimaendeleo na kufanya iendelee kunga'ra zaidi "Dodoma tumepata upendeleo wa kipekee wa kuwa na miradi mingi ,miaka 20 iliyopita Dodoma katikati eneo ambalo lilikuwa na kiwango cha lami ilikuwa ni ‘full street’ kuna wakati kulikuwa na shida kidogo leo ukizunguka katika Jiji la Dodoma katikati, eneo kubwa limezungukwa na Barabara yenye kiwango cha lami katika halmashauri zote nchi nzima, Jiji la Dodoma ndio linaongoza kwa mtandao mrefu wa Barabara za kiwango cha lami, sisi tuna Kilomita 249.12 hivyo Jiji la Dodoma ndio kinara kwa Tanzania nzima, nashukuru sana kwa kazi kubwa iliyofanyika kupitia miradi mbalimbali" alisema Mavunde
Nae Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Rosemary Senyamule, alisema kuwa amefurahishwa sana na utiaji saini huo kwasababu ni jambo ambalo sio la kawaida na husaidia kutatua changamoto za wananchi wa Jiji la Dodoma."Nipo hapa kushudia mkataba kwa ajili ya ujenzi wa miradi mikubwa ya kimkakati kwa Jiji la Dodoma haya mambo ni ya kushangaza lakini Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan ndiye Rais anaeyafanya haya" alisema Senyamule.
1 CDA Street, 40477
Anuani ya posta: 1249, DODOMA, TANZANIA
Simu: +255 26 232 4817
Simu ya kiganjani:
Baruapepe: cd@dodomacc.go.tz
Copyright ©2017 The City Council of Dodoma. All rights reserved.