Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii wa Jiji la Dar es Salaam amesimamishwa kazi kwa agizo la Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI anayeshughulikia Elimu, Mhe. Reuben Kwagilwa (Mb), kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Prof. Riziki Shemdoe, ili kupisha uchunguzi wa tuhuma za kukopesha fedha za Umma kinyume na taratibu, ikiwemo upotevu wa fedha hizo.
Agizo hilo limeekezwa kwa Katibu Mkuu OWM – TAMISEMI wakati wa kikao cha majumuisho ya ziara ya kikazi ya Mhe. Kwagilwa mkoani Dar es Salaam, ambapo amesema kuwa Bi. Fransisca Makoye alihusika kuruhusu mikopo isiyo na ufuatiliaji sahihi na pia alihusishwa na tukio la kikundi kilichopewa gari kwa mkopo kuamua kuliuza bila ridhaa ya mamlaka.
“Kikundi kilipewa gari kwa mkopo, lakini gari hilo limeuzwa wakati nyaraka zote ziko kwa maafisa wa Serikali hili halikubaliki, natoa maelekezo afisa huyu asimamishwe kazi mara moja kupisha uchunguzi,” Amesema Mhe. Kwagilwa.
Katika hatua nyingine ya kuimarisha uwajibikaji, Mhe. Kwagilwa ameelekeza Wakuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii wa Halmashauri ya Manispaa Kigamboni na Ubungo kurejeshwa kazini kutoka likizo ili watoe maelezo ya kina kuhusu fedha za mikopo ya asilimia 10 kwa Wanawake, Vijana na Watu wenye Ulemavu.
Aidha, ameagiza aliyekuwa Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii wa Manispaa ya Temeke atafutwe na arejeshwe kazini kusaidia uchunguzi wa upotevu wa fedha za mikopo ya asilimia 10 katika Halmashauri ya Manispaa hiyo.
1 CDA Street, 40477
Anuani ya posta: 1249, DODOMA, TANZANIA
Simu: +255 26 232 4817
Simu ya kiganjani:
Baruapepe: cd@dodomacc.go.tz
Copyright ©2017 The City Council of Dodoma. All rights reserved.