Na. OWM – TAMISEMI
Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) anayeshughulikia Afya, Dkt. Jafar Seif, amesema anakusudia kuzunguka nchi nzima kuzungumza na watumishi wa kada ya afya ngazi ya msingi ili kusikiliza changamoto zao na kujadiliana kwa pamoja juu ya namna bora ya utatuzi wa changamoto hizo, ikiwa ni sehemu ya kwanza ya uboreshaji wa huduma za afya nchini kuelekea mpango wa bima ya afya kwa wote.
Naibu Waziri, Dkt. Seif, ameyasema hayo wakati akizungumza na watendaji wa Hospitali ya Wilaya ya Makete mkoani Njombe alipofanya ziara ya ukaguzi wa mwenendo wa maboresho ya miundombinu na kukagua vifaa tiba vya kisasa vilivyonunuliwa na Serikali ya Awamu ya Sita kwa lengo la kusogeza huduma za kibingwa karibu na wananchi katika maeneo ya pembezoni mwa miji.
Amesema dhamira ya Serikali ni kuwahudumia Watanzania wote bila ubaguzi, akisisitiza kuwa kila Mtanzania ana haki ya kupata huduma bora kadri ya hitaji lake, na ili kulifanikisha hilo anakusudia kuwatembelea watendaji wa sekta ya afya nchi nzima ili kuzungumza nao katika muktadha wa kutatua changamoto zinazoweza kutafsiriwa kama kikwazo cha huduma bora katika maeneo yao ya kutolea huduma.
“Sisi kwa sisi tunapozungumza tupeane moyo, na mimi nitazunguka nchi nzima kuzungumza na watendaji wenzangu wa sekta ya afya kujua nini wanachokiona kama changamoto katika maeneo yao ya kutolea huduma kwa jamii na kusikiliza ushauri wao katika utatuzi wa changamoto husika, sisi wenyewe kama watendaji tunaomsaidia Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan tunaweza kuzitatua, changamoto zinazotuzunguka kwa kujadiliana na kukubaliana kwa pamoja, ninaamini hili linawezekana,” amesema Dkt. Seif.
Awali, Katibu wa Afya wa Hospitali ya Wilaya ya Makete Aderiko Dominick amempongeza Naibu Waziri Dkt. Seif kwa namna alivyotoa nafasi ya kusikiliza changamoto za watumishi wa kada ya afya na kada zingine katika wilaya ya Makete, akipongeza kile alichodai kuwa ni busara katika kuzungumza na watumishi wanaohudumu katika maeneo ya pembezoni ambayo kwa namna moja au nyingine yanakabiliwa na changamoto za kimazingira.
1 CDA Street, 40477
Anuani ya posta: 1249, DODOMA, TANZANIA
Simu: +255 26 232 4817
Simu ya kiganjani:
Baruapepe: cd@dodomacc.go.tz
Copyright ©2017 The City Council of Dodoma. All rights reserved.