Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) anayeshughulikia Elimu, Mhe. Reuben Kwagilwa (Mb), ameagiza kufanyika kwa tathmini ya kina ya mafunzo ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) yaliyotolewa kwa walimu, ili kubaini uwezo halisi wa walimu katika kutumia vifaa vya TEHAMA kufundishia.
Mhe. Kwagilwa ametoa maelekezo hayo Jijini Mbeya, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Mhe. Profesa Riziki Shemdoe, wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua maandalizi ya mapokezi ya wanafunzi wa kidato cha kwanza yanayotarajiwa kuanza Januari
Mhe. Kwagilwa amesema, bado kuna changamoto kwa baadhi ya walimu, hususan wa masomo ya Sayansi kushindwa kutumia mifumo na vifaa vya TEHAMA licha ya uwepo wake mashuleni, hali inayosababisha utegemezi kwa walimu wachache wenye ujuzi, ambao mara nyingi hawashirikishi wenzao.
“Haikubaliki vifaa hivi nchi nzima viwe vya maonesho, mgeni akija anaoneshwa, mgeni akiondoka, mwalimu hajui kutumia wala mwanafunzi hajui kutumia. Yafanyike mafunzo ya kina kwa walimu wote ili wamudu matumizi ya vifaa vya TEHAMA,” amesema Mhe. Kwagilwa.
Mhe. Kwagilwa amesisitiza kuwa, hali hiyo haikubaliki na kwamba ni lazima hatua za haraka zichukuliwe kuhakikisha walimu wote wanapatiwa mafunzo ya kutosha yatakayowawezesha kutumia vifaa vya TEHAMA katika ufundishaji na ujifunzaji.
Ameongeza kuwa, Serikali haitavumilia kuona uwekezaji mkubwa uliowekwa katika ununuzi wa vifaa vya TEHAMA mashuleni unakosa tija kutokana na uzembe au ukosefu wa mafunzo stahiki kwa walimu ambao wanapaswa kuvitumia vifaa vya TEHAMA kufundishia, akisisitiza kuwa matumizi sahihi ya TEHAMA ni nyenzo muhimu katika kuboresha elimu.
1 CDA Street, 40477
Anuani ya posta: 1249, DODOMA, TANZANIA
Simu: +255 26 232 4817
Simu ya kiganjani:
Baruapepe: cd@dodomacc.go.tz
Copyright ©2017 The City Council of Dodoma. All rights reserved.