Na. Aisha Ibrahim, UHURU
Wazazi na walezi wamekuwa na mchango mkubwa katika kupanda kwa kiwango cha ufaulu kwa wanafunzi kutokana na juhudi kubwa wanayoifanya ya kutoa michango na nafaka shuleni ili kuhakikisha wanafunzi wanapata lishe bora na kuongeza kiwango cha umakini jambo linalopelekea kupanda kwa kiwango cha ufaulu.
Kauli hiyo ilitolewa na Mwl. Sospeter Ramadhan, kutoka Shule ya Msingi Uhuru wakati akifafanua kuhusu utekelezaji wa ajenda ya lishe shuleni na umuhimu wake kwa waandishi wa habari waliotembelea shule yake kuona utekelezaji wa agenda ya lishe.
Alisema kuwa katika kuhakikisha wanafunzi wanasoma na kuelewa, shule hiyo imekuwa na ushirikiano wa hali ya juu na wazazi na walezi kutoa michango ya fedha na nafaka ili watoto wapate chakula, pia mchango wa mawazo kwa lengo la kuboresha kiwango cha elimu bora. “Wazazi na walezi wamekuwa mstari wa mbele kujitolea michango ya fedha na hata mawazo ili kuhakikisha watoto hawa wanapata chakula wawapo shuleni. Jambo hili ni hamasa kubwa na hupelekea wanafunzi wetu kufaulu vizuri. Watoto wetu wanapata lishe kama ifuatavyo; darasa la kwanza na la pili kwakuwa wanarudi nyumbani kwao ifikapo saa tano asubuhi wao wanapata uji wa lishe pekee. Kuanzia darasa la tatu mpaka la saba, kwakuwa wanatoka shule saa 10 jioni wao wanapata uji pamoja na chakula cha mchana” alisema Mwl. Ramadhani.
Kwa upande wake mwanafunzi wa darasa la sita shuleni hapo, Fathiya Saleh alisema kuwa kabla ya kuletewa mpango wa chakula shuleni, wanafunzi walikuwa wanashindwa kumsikiliza mwalimu vizuri pindi anapofundisha. “Kabla hatujaanza kupikiwa shuleni tulikuwa tukikaa darasani mchana tunaanza kusinzia kwasababu ya njaa na kushindwa kumsikiliza mwalimu akiwa anafundisha” alisema Saleh.
Aliongeza kuwa, anaishukuru serikali ya Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwapatia huduma ya chakula shuleni kwasababu kupitia mpango huo umeweza kuinua ufaulu wao kwa kiwango cha hali ya juu na pia aliahidi kusoma kwa bidii na kuweza kufaulu masomo vizuri.
1 CDA Street, 40477
Anuani ya posta: 1249, DODOMA, TANZANIA
Simu: +255 26 232 4817
Simu ya kiganjani:
Baruapepe: cd@dodomacc.go.tz
Copyright ©2017 The City Council of Dodoma. All rights reserved.